ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, September 16, 2017

MSEKWA ATIA NENO UTENDAJI KAZI WA SPIKA NDUGAI BUNGENI.


Spika mstaafu wa Bunge, Pius Msekwa ametia neno akigusia utendaji wa Spika wa Bunge, Job Ndugai aliyeingia katika msuguano na baadhi ya wabunge wa upinzani.


Ndugai ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Kongwa mkoani Dodoma hakuwa na wakati mzuri katika Bunge lililomalizika jana kutokana na kupishana kauli na wabunge, Zitto Kabwe, Said Kubenea, Godbless Lema na Peter Msigwa.

Alipotakiwa kutoa maoni yake kuhusu Spika Ndugai alivyojikuta akitumbukia katika mvutano huo, Msekwa alisema: “tulifundishwa na Mzee Mwinyi(Ali Hassan) kila kitabu na zama zake.”

Amesema ingawa wakati wa uongozi wake hakukuwa na malumbano ya namna hiyo lakini hilo halimanishi kuwa Spika wa sasa anaendesha mambo kinyume na Kanuni za Bunge.

Amesema anachokifanya Spika Ndugai kinatafsiri aina ya uongozi alionao ambao siyo jambo la kushangaza kuona ukitofautiana na mfumo aliokuwa akitumia wakati akiwa katika kiti hicho.

“Hii ni staili yake ya uongozi na ndiyo mabadiliko ya uongozi wenyewe,” amesema Msekwa wakati akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu na kurudia tena maneno hayo akisema “ ni staili yake na kila kiongozi anakuwa na mfumo wake wa kuongoza mambo.”

Lakini amesema kwa kufanya hivyo hajakosea lolote kwa vile yale aliyokuwa akiyazungumza na kuyatolea maamuzi yako ndani ya Kanuni za Bunge.
“Spika ametumia mamlaka yake sioni kama kuna ubaya wowote,” amesema Msekwa ambaye amewahi pia kuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM.

Amesema hata yeye alipochukua nafasi hiyo kulikuwa na maspika wengine waliomtangulia waliokuwa na mfumo wao wa kuendesha Bunge na kisha naye akawa na wake pia.
“Baada ya mimi walikuja wengine ambao nao pia walikuwa na staili yao ya uongozi,” amesema.

Hatua ya Ndugai kudai kuwa anaweza kumzuia Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe asizungumze bungeni kwa muda wote uliobaki na hana cha kumfanya imezusha mjadala mkubwa nchini huku baadhi ya wasomi wameikosoa kauli hiyo wakisema hana mamlaka hayo kisheria.

Spika Ndugai alitoa kauli hiyo hivi karibuni baada ya Zitto kunukuliwa katika akaunti yake ya Twitter akimkosoa kiutendaji.

Mzozo kati ya Spika Ndugai na Zitto ulianza baada ya kiongozi huyo wa ACT – Wazalendo kusema kwamba Bunge limewekwa mfukoni na mhimili fulani wakati alipotoa maoni kuhusu ripoti mbili za kamati ya Bunge za almasi na Tanzanite.

Kutokana na kauli hizo, Spika Ndugai aliagiza mbunge huyo ahojiwe na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge huku akimshtaki kwa wapigakura wake akisema licha ya kwamba mbunge wao yupo nchini hajafika bungeni kuwawakilisha na yeye (Spika), hana taarifa.

Wakizungumzia matamshi hayo baadhi ya wasomi walisema kauli kama hiyo haikupaswa kutolewa na Spika.
Baadhi ya wanasheria walisema kauli ya Spika Ndugai imelenga kuwanyamazisha wabunge wasiwe huru kutoa maoni yao kwa mujibu wa Katiba.

MAFUNZO YA SIKU 5 WAKUU WA WILAYA NA WAKURUGENZI WA MIKOA MINNE YAMALIZIKA DODOMA.

Mh. Selemani Jafo, alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tano kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mikoa minane kwenye ukumbi wa Hazina Mjini Dodoma.
Mh. Selemani Jafo, alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tano kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mikoa minane kwenye ukumbi wa Hazina Mjini Dodoma huku Wakiwa wanamsikiliza kwa makini.

Mh. Josephine Matiro Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga akitoa neon la Shukrani mara baada yakufungwa kwa mafunzo hayo.

 Bibi Zainabu Chaula, Naibu Katibu Mkuu Afya TAMISEMI, alipokuwa akitoa neon kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufunga Semina hiyo.
Baadhi ya Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya wakisikiliza kwa makini Hotuba ya Ufungaji wa Semina hiyo ya siku tano. (Picha zote na Idara ya Habari Maelezo- Dodoma)

VITUO VYA AFYA 172 KUKARABATIWA NA UBALOZI WA CANADA.



Jaffo-  “Mabilioni  Kwa Afya za Watanzania”
Na. Atley Kuni- TAMISEMI
Serikali imepanga kukarabati vituo vya afya 172 kutokana na fedha kutoka Benki ya Dunia na Ubalozi wa Canada ambapo wametoa jumla ya Dolla za Kimarekani Mil 88 sambamba na Bil.12 fedha za kitanzania zilizovuka katika mwaka wa fedha wa 2016/2017.

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mh. Seleman Jafo (Mb) amesema lengo la serikali nikuhakikisha ifikapo Desemba 30, 2017 shughuli hiyo iwe imekamilika ipasavyo kwa kusimamiwa karibu na Waheshimwa Wakuu wa mikoa wakisaidiana na Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya.

Jafo amesema kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Serikali imepokea Dolla za kimarekani  Mil. 66 kutoka Benki ya Dunia ambapo vituo 103 vitakarabatiwa aidha pia Serikali  kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI, imepata Msaada kutoka Ubalozi wa Canada wa dolla za kimarekani Mil 22, ambapo vituo 44 vya afya vitakarabatiwa kwa fedha hizo. 

Naibu waziri huyo alisema,  fedha zingine zitakazo tumika katika zoezi hilo ni zile zilizo vuka katika mwaka wa fedha uliopita.

“Vituo 25 vitafanyiwa ukarabati kupitia fedha za Benki ya Dunia na mfuko wa afya wa pamoja zilizovuka mwaka wa 2016/2017, ambapo Bil.12 za kitanzania zitatumika,” alisema Jafo na kuongeza  kwamba kila  “kituo kitapatiwa shilingi Mil. 500 za kitanzania na baada ya ukarabati serikali itakuwa na jukumu lakupeka vifaa katika maeneo hayo”.

Waziri Jafo amesema, Maeneo ya kipaumbele wakati wa ukarabati huo ni pamoja na  Upasuaji (Theater), Wodi za mama na Mtoto (Martenity), Maabara(Laboratory), pamja na Nyumba za watumishi sambamba na maeneo mengine ya kipaumbele kutokana na fedha zilizopo.

Katika hatua nyingine Jafo amewagiza Makatibu Tawala wa mikoa kuwasilisha Taarifa ya kila mwezi ofisini kwake juu ya maendeleo ya ukarabati, huku akiwataka Wakurugenzi na watendaji wengine kusimamia kwa ufasaha zoezi hilo. 

Naibu Waziri hakusita kuonya juu wale wote watakao kwenda kinyume na maagizo na maelekezo ya serikali yaliyotolewa.

“Nawaomba Wah. Wabunge na Madiwani kushirikiana bega kwa bega na watendaji katika kufanikisha zoezi hili kwa ufanisi, alisema Jafo na kuongeza kwamba,  “ofisi yangu haita mvumilia Kiongozi au Mtendaji yeyote atakaye onekana kutumia fedha hizo vibaya au kushindwa kutimiza wajibu wake na kisha kukwamisha shughuli hii muhimu yenye nia njema kwa maisha ya watanzania.

Akihitimisha maagizo hayo  Naibu waziri Suleima Jafo, amezishukuru  Wizara zote za kisekta katika kusukuma gurudumu la maendeleo  na kwenda sambamba na kasi ya Rais  Mh. Dkt. John Pombe Magufuli ya HAPA KAZI TU,  ikiwapo, Wizara ya Afya, Fedha na Mipango pamoja na watendaji wa Ofisi yake ambao walikuwa bega kwa bega katika mchakato wote wa kupatikana kwa fedha.

MADUDU YA ARDHI MWANZA: MKUU WA MKOA AMSIMAMISHA KAZI MTHAMINI WA ARDHI ILEMELA.

NA ZEPHANIA MANDIA


Mkuu wa mkoa wa Mwanza JOHN MONGELA ameanza jitihada za kuhakikisha anapunguza kama siyo kumaliza kabisa migogoro ya ardhi katika jiji la mwanza na manispaa ya Ilemela, maeneo ambayo kwa muda mrefu yamegubikwa na migogoro ya ardhi.


Jitihada hizo zimeanza katika Manispaa ya Ilemela na jiji la Mwanza ambako akiwa amefuatana na wataalam wa halmashauri ameweza kuhudumia mamia ya wanachi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakizungushwa bila ya kupata haki zao.


Mamia ya wananchi kutoka nyamagana na Ilemela baadhi yao wakiwa wamedhoofu kwa uzee na mahangaiko ya muda mrefu kutokana na kufuatilia haki ya ardhi waliyokuwa wakimiliki katika halmashauri, bila ya mafanikio. Hata hivyo Jitihada zilizoanzishwa na mkuu wa mkoa wa Mwanza JOHN MONGELA za kutafuta ufumbuzi zimerejesha tabasamu kwa wazee waliohangaika kwa zaidi ya miaka 20.


Wataalamu kitengo cha ardhi katika manispaa ya Ilemela na jiji la Mwz walikuwa na wakati mgumu kutoa majibu ya kero za wananchi.


ENGBERT REBUKABWE – MTHAMINI ARDHI Akaonja shubiri ya MONGELA        ambaye ni mkuu wa mkoa wa Mwanza.


Mwanza JOHN MONGELA amefanyakazi kwa zaidi ya saa 18 hadi saa sita usiku akisuluhisha migogoro ya ardhi katika manispaa ya Ilemela na siku iliyofuata amekuwa ktk wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza

HATUUNGI MKONO KOREA KASKAZINI, MARUFUKU KUNDAMANA KUMUOMBEA TUNDU LISSU, MBOWE: TUMECHUKUWA TAHADHARI ZOTE KUMLINDA LISSU, SPIKA: WABUNGE MSIKESHE BAA.


Hatuungi mkono Korea Kaskazini,Marufuku kuandamana kumuombea Tundu Lissu,Mbowe:Tumechukua tahadhari zote kumlinda Lissu, Spika: Wabunge msikeshe baa.Pata dondoo za magazeti ya leo hapa.

Friday, September 15, 2017

DEREVA WA MBUNGE HECHE AKATWA MAPANGA NA WATU WASIOJULIKANA


Dereva wa Mbunge John Heche amevamiwa usiku wa kuamkia leo na watu wasiojulikana na kukatwa mapanga Mjini Tarime majira ya saa 2 usiku na hali yake siyo nzuri.

Mbunge John Heche amethibitisha kutokea kwa tukio hilo kutokana na taarifa alizopata kupitia Katibu wake, Mrimi Zablon ambaye amekiri Dereva huyo anayefahamika kwa jina la Suez Daniel Maradufu ni kweli amepata shambulio hilo na sasa yupo hospitali akipatiwa matibabu.


Kwa upande wa Kamanda wa Polisi Tarime Rorya, SACP Henry Mwaibambe alipotafutwa kwa njia ya simu na Mwandishi wetu amesema yupo kwenye kikao na akimaliza atatoa ripoti kamili.


Dereva huyo amelazwa katika hospitali ya Bomani Tarime mkoani Mara.

OPARESHENI YA KUPAMBANA NA KIRUSI KINACHOSABABISHA ULEMAVU YAANZA TANZANIA.

Waratibu wa wilaya za mikoa ya Njombe, Mbeya na Iringa wametakiwa kuifikishia jamii mafunzo waliyopokea kwa takribani siku tatu juu ya kupambana na ugonjwa wa ulemavu wa ghafla unaosababishwa na kirusi hatari anaefahamika kwa jina la KIRUSIPOLI.

Agizo hilo limetolewa na Afisa mfuatiliaji wa magonjwa yanayozuilika kwa chanjo Honest Nyaki wakati akihitimisha mafunzo hayo yaliyotolewa kwa siku tatu mkoani njombe kwa waratibu wa wilaya ambayo yanalenga kuielimisha jamii jinsi ya kuepukana na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.

Zoezi la utoaji mafunzo linafanyika nchi nzima kwa lengo la kutokomeza na kuelimisha jamii hasa katika kuwa na ufahamu juu ya magonjwa ya ulemavu wa ghafla ambao dalili yake kuu ni mwili kulegea na kuwa tepetepe dalili ambayo inatambulisha ugonjwa huo wa ulemavu wa ghafla ambao unasababishwa na kirusi kinachofahamika kama KIRUSIPOLI ( POLIO VIRUS ) kinachopatikana na kwenye kinyesi.

TAARIFA NA AMIRI KILAGALILA

POLIOVIRUS ndio jina halisi la kirusi hicho ambacho kwa lugha ya kiswahili kinafahamika kama KIRUSIPOLI , Kwa mujibu wa mtaalamu ambae ni afisa ufuatiliaji wa magonjwa yanayozuilika kwa chanjo anasema kuwa kirusi huyu ni hatari na amekuwa akiwakumba hasa watoto walio na umri chini ya miaka kumi na mitano .

CUE....................................................MTAALAMU.

Aidha jamii imetakiwa kuchukua hatua za haraka pindi wanapoona mtoto anadalili hiyo kuu mwili kulegea na kuwa tepetepe basi wachukue hatua za kuripoti katika vituo vya afya ili hatua za vipimo ziweze kufuata kwaajili ya matibabu ya mtoto.

CUE ......................................................WITO KWA JAMII.

Mwaka 1996 nchini tanzania mgonjwa wa ulemavu wa ghafla alipatikana kwa mara ya mwisho ambapo mpaka sasa hakujatokea tena mgonjwa au mwathirika wa ugonjwa huo hali ambayo imewalazimu watalaamu kuchukua hatua za kufanya uchunguzi kwaajili ya kutafuta kama ugonjwa huu upo ili kuweza kuuteketeza kabisa kwaajili ya usalama wa afya za watoto.

CUE............................................................UKUBWA WA TAITIZO LA ULEMAVU WA GHAFLA

Pius Willium Yonga na Dr.Huruma ni miongoni mwa waratibu ambao wamehudhuria katika mafunzo hayo ya siku tatu hapa mkoani njombe , ambao wanasema kuwa wameyapokea mafunzo kwa mikono miwili huku wakiahidi kuyapeleka mafunzohayo kwa jamii na kueleza kuwa mafunzo hayo ni muhimu kutokana na mpango uliopo wa kutokomeza magonjwa ya ulemavu wa ghafla pamoja na surua nchini tanzania.

CUE............................................................WARATIBU.

Hata hivyo jamii imetakiwa kuwa na matumizi sahihi ya vyoo bora ili kuhakikisha kuwa kirusi cha ugonjwa wa ulemavu wa ghafla hakipewi nafasi katika kuwadhuru watoto.

Thursday, September 14, 2017

SERIKALI YAANZA JITIHADA ZA KUWAKABILI VIWAVIJESHI HATARI AINA YA FALL ARMYWORM (FAW)


 Kiwavijeshi aina ya Fall Armyworm (FAW)
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi, Bwana Beatus Malema akizungumza wakati akifungua warsha ya siku moja kujadili namna ya kukabiliana na mdudu aina ya Kiwavijeshi
Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Afya ya Mimea, Idara ya Maendeleo ya Mazao katika Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi, Bibi Beatrice Palangyo akiwasilisha mada ya utambuzi wa Viwavijeshi wapya aina ya Fall Armyworm (FAW) wanaojulikana kitaalamu kama Spodoptera Frugiperda wakati wa warsha ya kujenga uelewa juu ya wadudu hao


Viwavijeshi wapya aina ya Fall Armyworm (FAW) wakishambulia mazao aina ya mahindi
Wadau wa kilimo kutoka Shirika la Maendeleo la Watu wa Marekani Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi, USAD, ONE HACKER FUND, Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu Ukanda wa Kitropiki  (TPRI), Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), na Mradi wa WEMA wakimsikiliza Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi, Bwana Beatus Malema akizungumza wakati akifungua warsha ya siku moja kujadili namna ya kukabiliana na mdudu aina ya Kiwavijeshi
 Baadhi ya wadau wa kilimo wakifatilia warsha
Viwavijeshi wapya aina ya Fall Armyworm (FAW) wakishambulia zao la Mahindi
 
Na Mathias Canal, Dar es salaam 

Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi imeanza jitihada za kuwakabili Viwavijeshi wapya aina ya Fall Armyworm (FAW) wanaojulikana kitaalamu kama Spodoptera Frugiperda ambao wametajwa kuwa na uwezo mkubwa kuharibu mazao mbalimbali hususan mahindi ambayo ndio zao kuu la chakula nchini.

Imeelezwa kuwa Viwavijeshi hao wanapofika kwenye mazao hutoa kemikali ambayo huweza kudanganya mmea kuwa unashambuliwa na magonjwa kama ukungu au fangasi hivyo mmea unapohisi unashambuliwa na hayo magonjwa, hupunguza kinga dhidi ya wadudu hao hatari na kuwa rahisi kushambuliwa. 

Hayo yamebainishwa leo Septemba 14, 2017 na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao kutoka Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi, Bwana Beatus Malema wakati akifungua warsha ya siku moja mbele ya Wadau wa Kilimo ambao ni Shirika la Maendeleo la Watu wa Marekani USAD, ONE HACKER FUND, Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu Ukanda wa Kitropiki  (TPRI), Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), na Mradi wa WEMA .

Mkutano ulikuwa na lengo la kujenga uelewa wa pamoja kwa ajili ya kumkabili mdudu huyo aina ya Fall Armyworm (FAW) ambaye anashambulia mazao mbalimbali nchini hususani zao la mahindi.

Alisema Athari ya viwavi jeshi haishii kuharibu majani ya mimea pekee, wadudu hao wanapokula majani na kutengeneza sumu aina ya ‘firenide’ inayodhuru mifugo inapokula majani yaliyoathiriwa.

Bwana Malema amesema tayari Serikali imechukua juhudi za awali kukabiliana na mdudu huyo ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi juu ya utambuzi wa mdudu huyo kwa kuwataka Wananchi kung’oa mazao na kuyachoma pindi wanapobaini uwepo wa mdudu huyo.

Pia tayari dawa tatu zimepitishwa na Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi kupitia Taasisi ya uchunguzi wa Viatilifu (TPRI) zinazoangamiza wadudu hao ambazo ni Duduba 450, Mupacrone 500 EC na Match Save kutoka Kampuni ya Syngenta hivyo Wananchi wametakiwa kuzitumia haraka pindi wanapoona dalili za kuwepo wa wadudu hao shambani.

Bwana Malema amesema kuwa katika kipindi cha miaka mingi Tanzania imekuwa ikikumbwa na viwavijeshi aina ya African Armywarms ambapo mara zote imekuwa ikiwadhibiti wadudu hao wanapojitokeza kwa kuwapa kiuatilifu kinachosababaisha matumbo ya wadudu hao kujaa na hatimaye kuwasababishia vifo.

Ameongeza kuwa kwa mara ya kwanza Wizara ilipata taarifa ya uvamizi katika shamba la Mwekezaji mkubwa Wilayani Nkasi Mkoani Rukwa mwezi Machi 2017 na walipofuatilia na kupeleka sampuli maabara mdudu huyo alibainika kwa jina la  Spodoptera frugiperda au Fall arymworm ambaye ni hatari na amekuwa akiripotiwa katika maeneo mbalimbali duniani.

Kutokana na unyeti wa suala hilo Wizara ya Kilimo imewasiliana na  Shirika la Chakula Duniani (FAO), kwa ajili ya kuunganisha juhudi za pamoja ili kumdhibiti mdudu huyo kabla hajasambaa kwenye maeneo mengi nchini.

Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) katika taarifa yake imesema viwavijeshi hao aina ya Fall armyworm wameonekama pia katika nchi za Zimbabwe, Malawi, Msumbiji, Namibia Afrika ya Kusini na Zambia huku chanzo chake ikiwa ni nchini Marekani.

Kwa mujibu wa Redio ya Umoja wa Mataifa, FAO bado haijatangaza   kiwango kamili cha uharibifu katika nchi hizo, huku ikiongeza kuwa Shirika hilo na Wadau wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wamejadili  udhibiti wa viwavijeshi.

Naye Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Afya ya Mimea, Idara ya Maendeleo ya Mazao katika Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi, Bibi Beatrice Palangyo akiwasilisha mada ya utambuzi wa wadudu hao katika warsha hiyo amesema kuwa katika Nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara wadudu hawa walianza kuingia nchini Nigeria na kwa sasa wameenea katika nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania, Afrika kusini, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Malawi.

Alisema wadudu hao wanashambulia mazao ya jamii ya nafaka kama mahindi (Corn) wanauwezo wa kushambulia hata magugu pale wanapokosa mazao kama mahindi kwani hawali mazao mengine kama mboga na matunda, wanakula zaidi mahindi na magugu yanayofanana na mahindi.

Zaidi ya Mikoa 15 nchini ikiwemo Zanzibar imeripoti kuwepo kwa kadhia ya mdudu huyo hivyo asilimia 15 ya mazao jamii ya nafaka kama mahindi yameathiriwa, jambo ambalo kama lisingepatiwa ufumbuzi wa haraka, lingesababisha upotevu mkubwa wa mazao mashambani na kutishia upatikanaji wa chakula nchini.

BUNGE LAMKINGIA KIFUA SPIKA NDUGAI.


 Bunge Lamkingia Kifua Spika Ndugai...Kuhusu Kauli Aliyoisema Kuhusu Gharama za Ndege iliyompeleka Tundu Lissu Nairobi.

JIUNGE NASI KATIKA Facebook, Instagram, Youtube, Twetter,

GEITA HAPATOSHI.


Baadhi ya askari wa kikosi cha kutuliza Ghasia wakiwa kwenye Barabara ambayo inatoka mgodi wa dhahabu wa Geita GGM Wakati wa shughuli za kuwatawanya viongozi hao pamoja na wananchi ambao walikuwa wameandamana .
Wananchi na madiwani wakiwa wameweka Mawe kabla ya kutawanywa .
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita,Elisha Lupuga akiwa kwenye kikao wakati alipokuwa akielezea namna ambavyo wameweza kufukuzwa na jeshi hilo.
Mkuu wa Wilaya ya Geita Mwl,Herman Kapufi akizungumza na kutoa maelekezo ya namna ya kufanya wakati wa kikao hicho.
Baadhi ya wajumbe wa kikao hicho wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya wakati alipokuwa akiwakilisha  maamuzi ambayo wameyachukua.
Mkuu wa Mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga akiwasisitiza kutulia na kuachana na ghasia wasubilie meza ya mazungumzo na Naibu waziri wa Nishati na madini siku ya Jumatatu.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Geita Mponjoli Mwabulambo akisisitiza kutokukubaliana na madiwani juu ya tukio ambalo wamefanya siku ya leo.





 Picha na Maduka Online.


Jeshi la Polisi Mkoani Geita limelazimika kutumia mabomu ya machozi na kupiga risasi za moto hewani kwaajili ya kuwaondoa waandamanaji ambao walikuwa wakiongozwa na madiwani wa halmashauri mbili ambazo ni ya mji na Wilaya ya Geita ambao walikuwa wametanda kwenye barabara ya mgodi huo wakizuia magari kuingia na kutoka Kampuni ya uchimbaji madini ya  dhahabu ya Geita (GGM),wakishinikiza kulipwa deni wanaloidai GGM kiasi cha zaidi ya Dola Bilioni 12.65


Tukio hilo limetokea  leo (jana) majira ya saa mbili na nusu asubuhi wakati madiwani hao na wananchi  wakiwa wamefunga barabara ya mgodi wakishinikiza kulipwa deni hilo kufuatia maazimio ya kikao maalumu cha baraza la madiwani  kilichokeiti  juzi.

Azma ya kukata mawasiliano ya barabara na vyanzo vya maji zilianza saa 10.00 usiku ambapo madiwani waliweka mawe katika njia kuu za kuingia mgodini humo na kwenye chanzo cha maji kilichopo Nungwe.


Baadi ya madiwani ambao wamzungumza na Maduka online Joseph kwenye eneo la tukio baada ya kutawanywa na mabomu ya machozi   Sasembe   
Kaparatusi na Constantine Molandi ambaye ni makamu mwenyekiti wa halmashuri ya mji wa Geita  wamesema kuwa  walikubaliana jana (juzi) kwenye vikao vya  chama  ngazi ya wilaya na mkoa pamoja na baraza maalum kuwa leo watafanya maandamano ya amani kwa lengo la  kushinikiza kudai deni hilo huku wakilaani kitendo cha jeshi hilo kutumia nguvu kubwa.


“Tulikubaliana kwenye vikao ngazi  ya chama wilaya ,na mkoa na baraza maalum la madiwani  na uongozi wa wilaya pamoja  na mkoa  unafahamu  kuwa leo tunaandamana kudai haki lakini cha kushngaza  askari polisi wametutawanya  kwa mabomu “ alisema Kaparatus .


Kabla ya kutawanywa waaandamanaji hao,Mbunge wa jimbo la Geita Bw. Joseph Kasheku Msukuma ameiambia maduka online  kuwa amesikitishwa na Kamanda Mkuu wa Polisi kumtuhumu kuwa yeye ndiye mchochezi mkuu wa mgogoro huo.


“Nashangaa sana RPC anakuwa na chuki na mimi kwani kuwa Mbunge ni tatizo kwani ubunge alinipa yeye hata kama nikiacha ubunge nina maisha yangu na awezi kusema kuwa ccm ni kielele yani kweli sisi ni kielele”alisema Msukuma.


Ameonezea kuwa   kiasi cha fedha zinazodaiwa zinatakiwa kulipwa kwani zimekuwa za muda mrefu na zinaweza kusaidia katika swala la maendeleo.


Hata hivyo amemtaka  Kamanda Mponjoli kuomba radhi kwa Chama Cha Mapinduzi ccm  na kwa serikali kwa ujumla kutokana na kauli mbaya alizotoa, akiongeza kuwa ameidhalilisha chama hicho.


“Kwa kauli hiyo inadhihirisha wazi kuwa Polisi wanakuwa na upande wakati wanapoenda eneno la kazi na hilo halitakiwi na kwa kutuuliza kwa dhihaka iwapo sisi ni CCM ama siyi, hiyo kauli ni mbaya sana kwani sisi tulikuwa tukidai haki ya kodi hiyo kwa niaba ya wananci wetu.


Mkuu wa Mkoa wa Geita, Meja Jenerali mstaafu Ezekiel Kyunga, ambaye aliwalaumu madiwani hao kwa kitendo cha kukata bomba la maji katika chanzo cha maji cha Nungwe, aliingilia kati suala hilo akashauri kuwa ni vyema shauri hilo likamalizwa kwa kutumia busara kwa manufaa ya wana Geita.


“Waheshimiwa Madiwani tuweke mbele hekima na busara, tuweke mbele huduma za jamii,  za mgodi wa GGM na wananchi kwa jumla ziendelee kwa amani hebu tuwe watulivu wakakti tukitafuta suluhu, kudai haki ni sawa lakini ni njia zipi mnatumia kuzidai, tuache kudai haki kwa njia ya fujo ya aina hii kwani sheria za nchi haziruhusu,”alisema.


Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Geita Mwl..Herman Kapufi amesema suala hilo limefikishwa katika wizara ya nishati na madini na kwamba jumatatu ya wiki ijayo Naibu waziri akiambatana na Kamishina wa madini watafika mkoani Geita kukutana na pande zote kwaajili ya kutafuta suluhu


 “Hata hivyo tumewasiliana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Mendrad  Kalemani juu ya suala hili ambapo tumekubaliana kukutana jumatatu ijayo, akiambatana na Kamishna wa madini  ambapo tutakaa nao pamoja na GGM  ili kujadili suala hili”Alisema Kapufi.


Licha ya ahadi hiyo ya Viongozi kutoka kwenye wizara husika, Mwenyekiti wa chama cha Mapinduzi CCM wilaya ya Geita Barnabas Mapande akaomba kutoa taarifa kwa mkuu wa wilaya kuwa kamanda wa jeshi la Polis mkoani humo anawatetea wawekezaji hasa GGM ambao wameshindwa kulipa fedha za kuharakisha maendeleo ya Mkoa


Naye Mkuu wa mkoa huo Meja jenerali mstaafu Ezekiel Kyunga,amesema njia pakee ya kumaliza mgogoro huo ni kufuata sheria,kanuni na taratibu bila kuathiri shughuli za kijamii na huduma kwa wananchi na kwamba njia iliyotumiwa na madiwani kudai haki yao si sahihi.


Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita,Mponjoli Mwabulambo amesema hayupo tayari kuomba radhi kwani swala hilo na mkusanyiko huo umefanyika kinyume cha sheria na kwamba hakuna lugha ambayo ametumia kukikashifu chama cha mapinduzi CCM.

IMEANDALIWA NA MADUKA ONLE.