ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, January 4, 2017

TRUMP AMUONYA OBAMA DHIDI YA KUWAHAMISHA WAFUNGWA WA GUANTANAMO..

Rais mteule wa Marekani Donald Trump amemuonya rais anayeondoka wa nchi hiyo Barack Obama juu ya kuwahamisha wafungwa wa jela ya Guantanamo iliyoko nchini Cuba.
Trump ameandika katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter  kuwa:  "Hakuna kuwahamisha wafungwa zaidi wa Gitmo, hawa ni watu hatari ambao hawafai kuachwa warejee katika uwanja wa mapambano."  

Mwezi uliopita, Josh Earnest, msemaji wa Ikulu ya White House ya Marekani alisema kuwa, serikali itafanya uhamisho wa mwisho wa wafungwa Guantanamo kabla ya kuondoka madarakani Rais Obama Januari 20. Iliarifiwa kuwa wafungwa hao watakabidhiwa serikali za Italia, Oman, Saudi Arabia na Imarati.
Jela ya Guantanamo iliyoko Cuba.
Mwezi Agosti mwaka uliopita, Wizara ya Ulinzi ya Marekani (Pentagon) iliwahamisha wafungwa 15 wa jela ya kutisha ya Guantanamo na kuwapeleka katika Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), ukiwa ni uhamisho mkubwa zaidi wa wafungwa hao kufanywa na utawala wa Rais Barack Obama wa Marekani.

Mara kwa mara shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limekuwa likikosoa vikali mienendo mibaya ya Marekani dhidi ya wafungwa wa jela hiyo na kusisitiza kuwa,  kuwanyima huduma za lazima kama matibabu wafungwa wa Gitmo, kunadhihirisha ni kwa kiasi gani serikali ya Washington isivyoheshimu mikataba ya kimataifa. Aidha Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Kupiga Vita Utesaji huko nyuma iliilaani Marekani kwa kukataa kuchunguza vitendo vya utesaji na unyanyasaji unaofanyiwa washukiwa wa ugaidi katika jela ya Jeshi la Marekani ya Guantanamo Bay.
Donald Trump (kulia) na Barack Obama.
Rais Barack Obama wa Marekani Januari mwaka 2009 aliahidi baada ya kushinda uchaguzi kuwa katika muda wa mwaka mmoja angeifunga jela ya Guantanamo, ahadi ambayo ameshindwa kuitekeleza hadi sasa ambapo anaondoka madarakani.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.