ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, December 17, 2016

MAHAKAMA YATUPA PINGAMIZI LA SERIKALI KATIKA KESI YA MBUNGE LEMA

RUSHA: Mahakama Kuu Kanda ya Arusha imetupilia mbali pingamizi la mawakili wa serikali ilizoweka dhidi ya taarifa ya dharura ya kusudio la kukataa rufaa ya mawakili wa Mbunge wa Arusha Mjini, Godblees Lema.
Jaji Modesta Opiyo wa mahakama kuu kanda ya Arusha alisema katika maamuzi yake kuwa pingamizi zilizowekwa hazina msingi kwani waleta maombi walifuata taratibu zote  katika kiapo na hati ya dharua ya kuitwa mahakamani.

Baada ya uamuzi huo Jaji Opiyo aliwataka mawakili wa Lema ,Shedrack Mfinanga na Faraji Mangula kuwasilisha hoja zao katika kiapo na hati ya dharura.

Akizungumza baada ya kukubaliwa na Jaji ,wakili Mfinanga alimtaka Jaji huyo kusikiliza rufaa hiyo kwani kuchelewa siyo sababu ya msingi sana kwa mujibu wa sheria na kunukuu kesi mbalimbali zilizochelewa kukatiwa rufaa kwa siku nyingi na kudai kuwa mahakama ya rufaa ilizikubali na kuzitolea maamuzi.

Mfinanga alisema na kumwomba Jaji kusikiliza rufaa yao kwa sababu ni ya msingi na kamwe haiwezi kuvunja sheria ya makosa ya jinai iliyowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mawakili wa serikali wakiongozwa na Wakili Mfawidhi Materius Marandu, Hashim Ngole na Elizabert Swai walipinga vikali kukubaliwa kwa rufaa hiyo kwa madai kuwa Jaji Msengi alitupilia mbali na kurudia kuikubali ni ukiukwaji mkubwa wa sheria za makosa ya Jinai.

Baada ya malumbano hayo yaliyochukuwa zaidi ya masaa 5  Jaji Opiyo alisema kuwa uamuzi wa kuikubali ama kuikataa rufaa hiyo atautoa Desemba 20 mwaka huu majira ya saa 6 mchana katika mahakama hiyo.

Lema anakabiliwa na kesi hiyo ya uchochezi aliyosomewa katika mahakama ya wilaya ya Arusha mbele ya hakimu mkazi Deusdedit Kamugisha Novemba 8 mwaka huu na aliwekewa pingamizi na mawakili wa serikali ya kutopata dhamana baada ya hakimu kusema kuwa dhamana iko wazi.

Mbunge huyo wa Arusha Mjini alikamatwa Novemba 2 mwaka huu Mkoani Dodoama kwa kosa hilo baada ya kuhutubia katika mikutano ya hadhara katika kata mbalimbali za Jiji la Arusha kuwa ameoteshwa kuwa Rais Magufuli atakufa kabla ya mwaka 2020 hali inayodaiwa kuleta uchochezi kwa wananchi waliomchagua kuwa Rais wa nchi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.