ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, July 2, 2016

RUFANI YA SHEIKH PONDA YAKWAMA MAHAKAMA KUU

RUFANI ya Jamhuri kupinga hukumu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro kumwachia huru Sheikh Ponda Issa Ponda, dhidi ya kosa la kushawishi wakazi wa mkoa huo kufanya kosa, ilikwama kuendelea jana na kuahirishwa kwa wiki tatu baada ya mawakili wa utetezi kuomba muda wa kujadili na mteja wao.

Jana kesi hiyo ilitajwa na Jaji Edson Mkasimongwa katika Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam.

Wakili wa Serikali Malangwe Mchungahela alidai kuwa kesi hiyo ilipangwa kutajwa jana kwa ajili ya kupanga tarehe ya kuanza kusikiliza.

Hata hivyo, mawakili wa utetezi, Abubakar Mohammed na Juma Nassoro, kwa nyakati tofauti waliomba mahakama kuwapa muda wa kuzungumza na Sheikh Ponda, kama wataendelea kutoa huduma kwake ama la.

Nassoro alidai kuwa makubaliano yao ya awali ya kumtetea katika mahakama ya chini yalishamalizika, na hakuna maelekezo yoyote ili kuweza kumuwakilisha mahakamani hapo. Jaji Mkasimongwa alisema kesi hiyo itasikilizwa Julai 23.

Katika rufani hiyo, upande wa Jamhuri uliwasilisha hoja nne ikiwemo, mahakama ya chini ilikosea kwa kutokuzingatia uzito wa ushahidi wa kielektroniki katika kutoka uamuzi wake.

Sababu ya pili na ya tatu, Jamhuri inadai, Hakimu wa Mary Moyo alikosea aliposema hati ya mashtaka ilikuwa na mapungufu ya kisheria na Sheikh Ponda hakuwa na nia ya kushawishi umma wa mkoa huo kufanya kosa siku ya tukio.

Sababu ya mwisho ya Jamhuri katika kupinga kuachiwa huru kwa Sheikh Ponda ni kwamba hakimu alikosea kusema kuwa ilishindwa kuthibitisha kosa bila kuacha shaka.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.