ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, July 30, 2016

KAKA WA RAIS MAGUFULI AFARIKI

KAKA wa Rais Dk. John Magufuli, Anthon Lubambagwe, amefariki dunia kutokana na maradhi ya kifua.
Taarifa ya kufariki kwa Lubambagwe ilitolewa jana na msemaji wa familia, Nebart Mlambi, aliyeeleza kuwa marehemu huyo alifariki saa 8:30 mchana katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Sekou Toure, jijini Mwanza alipokuwa amelazwa akitibiwa.

Mlambi alisema marehemu Antony ni mtoto wa Helman Gwape Lubambagwe ambaye ni baba mkubwa na Rais Magufuli.

“Mzee alianza kuugua Aprili mwaka huu na kutibiwa katika Kituo cha Afya cha Igoma, akapata nafuu lakini alizidiwa tena Julai 27, mwaka huu tukampeleka Hospitali ya Sekou Toure.

“Alipokelewa pale lakini hali yake iliendelea kuwa mbaya wakamhamishia chumba cha wagonjwa mahututi ambako alifariki,” alisema Mlambi.

Taarifa kutoka ndani ya familia ya Rais Magufuli zimeeleza kuwa marehemu Anthon ndiye aliyempokea Rais Magufuli na kuishi naye wakati akianza masomo katika Shule ya Sekondari ya Lake jijini Mwanza.

Wakati Rais Magufuli akijiunga na Shule ya Sekondari ya Lake, marehemu alikuwa akiishi Mtaa wa Majembe Makali uliopo Kata ya Igogo na baadaye alihamia Mtaa wa Kishiri akiwa pamoja na Rais Magufuli.

Aidha, mtoto mkubwa wa marehemu huyo, Masumbuko Anthon (30), alisema maziko ya baba yake yatafanyika leo (Jumamosi) katika makaburi ya familia yaliyopo Igelegele, Kata ya Mahina, wilayani Nyamagana, ikitanguliwa na Ibada ya Misa itakayofanyika nyumbani kwake Kishiri, Kata Igoma ambako mwili wake utaagwa.

Marehemu ameacha mjane, Selina Masanja (60) na watoto saba ambao ni Masumbuko (30), Helman (34), Anna (28), Dotto (28), Paschal (26), Shija (22) na Mitimingi (12).

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.