ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, March 25, 2016

SIKU SABA NGUMU KWA DR. SHEIN.

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu jana alimwapisha Dk Ali Mohamed Shein kuwa Rais wa Zanzibar na hivyo kufungua siku saba ngumu kwa kiongozi kuunda Serikali itakayokidhi mahitaji ya Katiba.

Dk Shein aliyeapishwa baada ya kutangazwa mshindi katika uchaguzi wa marudio, atalazimika kwa mujibu wa Ibara ya 39 (2) ndani ya siku saba kuanzia jana, kuteua makamu wa kwanza wa Rais na makamu wa pili wa rais.

Kwa mujibu wa Katiba hiyo ya mwaka 1984, Toleo la 2010, uteuzi huo unatakiwa kufanyika baada ya Rais huyo kushauriana na chama kilichoshika nafasi ya pili katika matokeo ya kura baada ya uchaguzi iwapo kitakuwa kimetimiza asilimia 10 ya kura zote za rais.

Hata hivyo, kwa kuwa hakuna chama kilichotimiza asilimia 10 ya kura zote, Dk Shein atalazimika kuteua makamu wa pili kutoka CCM na kuacha nafasi ya makamu wa kwanza kwa kuwa vyama vyote vilivyoshiriki uchaguzi havina sifa za kupendekeza jina makamu huyo atakayeshika nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Maalim Seif Sharif Hamad.

Vilevile, kutokana na wapinzani kutotimiza vigezo hivyo, baada ya muda huo Rais huyo kwa mujibu wa Ibara ya 39 A (2) ya Katiba hiyo atalazimika kuwateua mawaziri na kuacha wazi nafasi za uteuzi wa chama au vyama vya upinzani.

Kibarua hicho kinamkuta Dk Shein huku ikiwapo ibara ya 9 (3) ya Katiba ya Zanzibar inayoeleza kuwa, “Muundo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar utakuwa wa Umoja wa Kitaifa na utendaji wa kazi zake utafanywa katika utaratibu utakaohakikisha kuendelezwa kwa umoja nchini na lengo la kufikia demokrasia.”

Kiapo
Dk Shein alikula kiapo cha kulinda Katiba saa 4.59 asubuhi katika Uwanja cha Amaan, Unguja mbele ya jopo la majaji, viongozi wa dini, wazee na wanasheria.

Dk Shein alisema atalinda na kutetea katiba zote mbili ya Zanzibar na ile ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania pamoja na kuwa mwadilifu.

Baada ya Jaji Mkuu kumlisha kiapo, alimkabidhi Katiba ya Zanzibar na ya Muungano ambazo ni mwongozo wa utekelezaji na uendeshaji wa nchi.

Hotuba
Katika hotuba yake ya kwanza baada ya kuapishwa, Dk Shein aliahidi kushirikiana kwa kila hali na vyama vya upinzani vilivyoshiriki uchaguzi wa marudio kwa lengo la kuleta maendeleo visiwani humo na Tanzania kwa ujumla.

“Utayari wenu wa kushirikiana na Serikali umenipa moyo, nami nawaahidi kuwa nitakuwa tayari kushirikiana nanyi katika kuwatumikia wananchi kuijenga nchi bila ubaguzi wowote kwani mimi ni Rais wa Wazanzibari wote,” alisema Dk Shein.

Kiongozi huyo aliwataka wananchi kuweka kando masuala ya uchaguzi na kujikita kwenye shughuli za kujenga uchumi ili kuleta maendeleo.

Katika kufanikisha hilo, Dk Shein aliahidi kuunda Serikali itakayozingatia nidhamu na utendaji utakaokuwa na tija kwa wananchi.

“Nitahakikisha Serikali nitakayounda itaendelea kushirikiana na ile ya Dk John Magufuli ili kuhakikisha wananchi wanaishi kwa amani na tunaendelea kushirikiana katika masuala yote ya maendeleo na kiuchumi,” alisema.

Dk Shein ambaye aliwasili katika uwanjani hapo saa 4.40 asubuhi alianza kwa kukagua gwaride na kisha kuelekea katika eneo maalumu la kiapo.

Alionya kuwa Serikali ya Zanzibar kwa kushirikiana na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haitamvumilia mtu au kikundi chochote kitakachoashiria kuleta uvunjifu wa amani nchini.

“Hatutomdhulumu mtu yeyote katika kutenda haki ila kubwa zaidi ninawanasihi wanasiasa pamoja na wanadini kuendelea kuitangaza amani iliyopo nchini ili isipotee kwa masilahi ya jamii na Taifa,” alisema.

Nderemo na shamrashamra zilitawala uwanjani hapo tangu asubuhi huku rangi za njano na kijani zikipamba kila kona.

Dakika 14, kabla ya Dk Shein kuwasili, Rais Magufuli aliingia uwanjani hapo ujio ulioamsha shangwe na vifijo kutoka kwa wanachama na mashabiki wa CCM.

Wimbo wa ‘Mpewa hapokonyeki aliyepewa kapewa’ uliopigwa na kikundi cha Cultural, ulionekana kuwa kivutio kwa watu wengi waliojitokeza katika sherehe hizo.

Mbali na Dk Magufuli, wengine waliohudhuria sherehe hizo ni Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na marais wastaafu Amani Abeid Karume (Zanzibar) na Ali Hassan Mwinyi.

Imeandikwa na Haji Mtumwa, Hassan Ali, Kalunde Jamal na Elizabeth Edward    

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.