ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, March 14, 2015

MAKAMU WA RAIS DKT. BILAL AIWAKILISHA TANZANIA KATIKA MKUTANO WA KIUCHUMI NA MAENDELEO WA MISRI (EGYPT THE FUTURE).

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akihutubia katika mkutano wa Kiuchumi na maendeleo wa Misri, uliofunguliwa jana Machi 13, 2015 na Rais wa Misri, Abdel-Fattah El- Sisi, mjini Sharm El-Sheikh, Misri. Picha na OMR
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, (katikati) akiwa na baadhi ya viongozi kutoka mataifa mbalimbali wakati akiwa katika mkutano wa Kiuchumi na maendeleo wa Misri, uliofunguliwa jana Machi 13, 2015 na Rais wa Misri, Abdel-Fattah El- Sisi, mjini Sharm El-Sheikh, Misri. Picha na OMR
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na Wawekezaji wa Misri wanaotaka kuwekeza katika Sekta ya Viwanja Wilayani Mkuranga, wakati alipokutana nao kwa mazungumzo leo, Machi 14, 2015 mjini Sharm El- Sheikh, Misri, alikohudhuria mkutano wa Kiuchumi na maendeleo wa Misri, uliofunguliwa jana Machi 13, 2015 na Rais wa Misri, Abdel-Fattah El- Sisi, mjini Sharm El-Sheikh, Misri. Picha na OMR
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akisalimiana na Rais wa Misri, Rais wa Misri, Abdel-Fattah El- Sisi, wakati walipokutana kwa mazungumzo baada ya mkutano huo, uliofanyika jana Machi 13, 2015 mjini Sharm El-Sheikh, Misri. Picha na OMR
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiagana na wageni wake Wawekezaji wa Misri wanaoataka kuwekeza katika Sekta ya Viwanda Wilayani Mkuranga, baada ya mazungumzo yao yaliyofanyika leo Machi 14, 2015 mjini Sharm El- Sheikh, Misri alikohudhuria mkutano wa Kiuchumi na maendeleo wa Misri, uliofunguliwa jana Machi 13, 2015 na Rais wa Misri, Abdel-Fattah El- Sisi, mjini Sharm El-Sheikh, Misri. Picha na OMR



 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MHESHIMIWA MAKAMU WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA AIWAKILISHA TANZANIA KATIKA MKUTANO WA KIUCHUMI NA MAENDELEO WA MISRI (EGYPT THE FUTURE)
SHARM EL SHEIKH, MISRI MACHI 14, 2015
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib Bilal jana Machi 13, 2015 ameiwakilisha Tanzania katika Mkutano wa Kimataifa wa Kiuchumi na Maendeleo nchini Misri. Mkutano huo umeandaliwa na Rais wa Misri Mheshimiwa Abdel Fattah Al Sisi na umehudhuriwa na viongozi karibu wote kutoka katika nchi za Kiarabu, marais na viongozi wakubwa wa nchi mbalimbali za Afrika pamoja na wakuu wa vyombo mbalimbali vya Kimataifa akiwemo pia Waziri wa Mmabo ya Nje wa Marekani John Kerry.

Akizungumza katika Mkutano huo, Rais wa Misri aliueleza ulimwengu kuwa Misri imepita jaribio kubwa na sasa iko imara tayari kusonga mbele hivyo wale wote walio na nia ya kuwekeza nchini Misri wafanye hivyo kwa kuwa serikali yake itashirikiana nao katika kuwalinda wao na mali zao. Pia Rais Sisi alifafanua kuwa, nchi yake inarejesha heshima yake iliyokuwa nayo zamani kutokana na mchango wake katika Umoja wa nchi za Kiarabu huku pia akisisitiza kuwa Misri sasa inarejea Afrika ambako anatambua kuna ndugu wa dhati.

Akihutubia mkutano huo Mheshimiwa Makamu wa Rais Dkt. Mohammed Gharib Bilal aliishukuru Misri kwa kuialika Tanzania kuhudhuria mkutano huo na akafafanua kuwa Tanzania inafurahia uamuzi wa Misri wa kujijenga upya huku ikikumbuka historia ya kutaka kujiwekea nafasi yake katika Afrika na katika nchi za Kiarabu.

“Mheshimiwa Rais, uitishaji wako wa mkutano huu mkubwa ni kiashirio kuwa sasa Misri inajijenga upya na kwamba inarejesha heshima yake katika Bara la Afrika, Nchi za Kiarabu na Dunia kwa ujumla,” alisema Mheshimiwa Dkt Bilal na kuendelea kuwa:

“Tunakupongeza kwa uongozi thabiti uliouonesha hadi sasa ambapo Misri inaonekana kuwa imara na thabiti. Uhusiano wetu ni wa kihistoria hivyo Tanzania inakupongeza na inaahidi kushirikiana nanyi katika ujenzi mpya wa Taifa lenu.”

Mheshimiwa Makamu wa Rais pia alitumia nafasi hiyo kuueleza mkutano huo kuwa eneo ilipo Misri linaunganisha Afrika, Nchi za Kiarabu na Ulaya na Tanzania nayo iko katika eneo la kitajiri kijiografia ambapo ukiwekeza nchini Tanzania unakuwa unapata fursa za ziada za kuwekeza katika nchi za Afrika Mashariki na nchi za Kusini mwa Afrika.

 “Ukiwekeza Tanzania utakuwa na uhakika wa soko la watu wasiopungua milioni 400 na nchi zetu ni lango la nchi zipatazo nane ambazo hazina bahari,” mheshimiwa Makamu wa Rais alisema na kufafanua kuwa Tanzania inakaribisha wawekezaji kama ambavyo Misri inafanya na zaidi akaeleza kuwa fursa za uwekezaji Tanzania ni nyingi na hasa sasa ambapo tunaelekea kuwa nchi ya uchumi wa kati.

Katika mkutano huu, Mheshimiwa Makamu wa Rais alipata nafasi ya kukutana na Mheshimiwa Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi na kuzungumza naye na kisha kuhudhuria mada ya kiuchumi iliyowasilishwa na Waziri Mkuu wa Misri Ibrahim Mahlab. Mheshimiwa Makamu wa Rais na msafara wake wanarejea nyumbani kesho tayari kuendelea na majukumu mengine ya Kitaifa.
 Imetolewa na: Ofisi ya Makamu wa Rais
           Sharm el Sheikh, Machi 14, 2015

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.