ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, July 19, 2014

KAA TAYARI KUSHUHUDIA KIVUMBI CHA PEPSI KOMBE LA MEYA 2014.

Mstahiki Meya wa jiji la Mwanza Mhe. Stanslaus Mabula (wa pili toka kushoto) akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) juu ya kuelekea kuanza kwa Michuano ya kandanda ya Pepsi Kombe la Meya 2014 , kutoka kushoto katika picha anaonekana meneja wa Kampuni ya SBC watengenezaji wa kinyaji cha Pepsi Nicolas Coetz, Balozi wa Habari wa Pepsi Kombe la Meya 2014, na meneja mauzo wa kampuni ya Pepsi Sharif Taki. 
MASHINDANO ya Pepsi Kombe la Meya Jiji la Mwanza 2014 kuanza kutimua vumbi Agosti 2 mwaka huu na Bingwa kujinyakulia mzigo wa kitita cha Sh. Milioni sita, wilayani Nyamagana mkoani Mwanza.
Mwaka huu jumla ya timu 22 zitashiriki ambapo timu 12 zitatoka katika Kata 12 za  Jimbo la Nyamagana na timu nyingine 12 zitatoka katika vikundi na asasi mbalimbali za kijamii zilizopo jimboni humo.

Balozi wa Habari wa Pepsi Kombe la Meya 2014, Albert G. Sengo akizungumza na wanahabari kuhusiana na taratibu za michuano hiyo zitakavyokuwa.
Mashindano haya yanafanyika kwa mwaka wa pili mfululizo chini ya udhamini wa Kampuni ya SBC inayotengeneza vinywaji baridi kupitia kinywaji chake cha Pepsi ambapo kwa mwaka huu yameboresha zaidi kwa kuhakikisha vifaa vitakavyotolewa vinakuwa na ubora ikiwa pia na ongezeko la ukubwa wa zawadi za washindi. “Lengo kubwa la mashindano haya ni kuwezesha vikundi vya vijana wajasiriamali, kuleta umoja, hamasa, kuendeleza vipaji vya soka, mshikamano na burudani, lakini pia kuviwezesha mitaji ya kuendesha shughuli zao kupitia mashindano ya soka ili kuvijengea uwezo,” BOFYA PLAY KUSIKILIZA.

Zawadi kwa washindi mwaka huu zimeongezeka ambapo bingwa atajinyakulia Bajaji ya kisasa ya kubeba mizigo na watu wanne yenye thamani ya milioni 4.5 na fedha tasilimu milioni 1.5 (jumla milioni sita), mshindi wa pili milioni 2, mshindi wa tatu milioni 1 huku mfugaji bora, timu yenye nidhamu na mwamuzi bora kuzawadiwa Sh. Laki mbili.
Awali meneja wa kamati ya mashindano ya Pepsi Kombe la Meya 2014, Bitegeko (wa kwanza kulia) alieleza kwamba timu zitakazoshiriki michuano hiyo zimegawanywa katika makundi manne ambapo kundi A litakuwa na timu sita, kundi B, C na D kila moja litakuwa na timu tano, mzunguko wa kwanza utachezwa kwa mtindo wa ligi katika makundi na hatua ya robo fainal timu zitacheza kwa mtoano hadi kupata timu mbili zitakazo cheza fainali ili kumpata bingwa kwa mwaka 2014.

“Viwanja vitakavyotumika katika michuano ya Kombe hilo ni Nyamagana, Nyegezi Kona, Mabatine Polisi, Buhongwa, Igoma Mnadani na Mkolani na waamuzi watakaochezesha mashindano hayo ni vijana wanafunzi kutoka katika Kituo cha Michezo cha Alliance cha jijini hapa,” alieleza.
Mstahiki Meya wa jiji la Mwanza Mhe. Stanslaus Mabula (wa pili toka kushoto) akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) juu ya kuelekea kuanza kwa Michuano ya kandanda ya Pepsi Kombe la Meya 2014 , kutoka kushoto katika picha anaonekana meneja wa Kampuni ya SBC watengenezaji wa kinyaji cha Pepsi Nicolas Coetz, Balozi wa Habari wa Pepsi Kombe la Meya 2014, na meneja mauzo wa kampuni ya Pepsi Sharif Taki. 
Moja kati ya kanuni za mashindano ya Pepsi Kombe la Meya 2014, zinaeleza kuwa timu itaruhusiwa kusajili wachezaji wasiozidi 25 kwa fomu zilizotolewa, Wachezaji wa Ligi kuu ya Vodacom na Ligi Daraja la Kwanza hawataruhusiwa katika mashindano haya.

Ni kosa kumchezesha mchezaji ambaye hajasajiliwa. Timu itakayo mchezesha mchezaji ambaye hayupo kwenye orodha ya wachezaji waliosajiliwa itapoteza michezo yote ambayo mchezaji huyo aliichezea.

Mchezaji hatoruhusiwa kusajiliwa kwenye timu zaidi ya moja. Iwapo mchezaji huyo akibainika ataondolewa kwenye mashindano na timu hiyo haitoruhusiwa kuweka mchezaji mwingine mbadala, timu itanyang'anywa pointi kwa michezo aliyo cheza mchezaji huyo.
Pepsi Kombe la Meya 2014 itafuata sheria zote 17 za soka. Kubadili wachezaji (substitution) mwisho watano. Mchezaji akipewa kadi nyekundu hatoruhusiwa kucheza mechi moja inayofuata. 

Mashindano yatasimamiwa na Kamati ya Mashindano ambayo inamamlaka ya kuifuta katika mashindano timu yoyote ambayo wachezaji wake watakuwa ni chanzo cha vurugu katika mashindano.
"Matayarisho yako safi kwa asilimia 100" says Nicolas Coetz.
*    Kila timu ina wajibu wa kutunza nidhamu ya wachezaji na washabiki wake ndani na nje ya mchezo.
*       Maamuzi ya refa yatakuwa ya mwisho katika mchezo.
*      Ni kapteni wa timu pekee ndiye anaruhusiwa kupeleka malalamiko kwa muamuzi ndani ya mchezo.
*    Timu itakayogomea mchezo itakuwa imepoteza mchezo husika na Kamati ya mashindano itakaa kuijadili timu hiyo kwa adhabu nyingine kama itaona inafaa.
*     Mchezo utaanza saa 10:30 jioni. Kila timu inatakiwa kufika uwanjani saa moja kabla ya mchezo kuanza.
*  Viongozi wa timu watatakiwa kusaini kwenye nakala ya kanuni itakayobaki kwa muandaaji wa mashindano ikiwa ni ishara ya kuwa wamezielewa na wataziwasilisha vyema kwenye timu zao ili kuboresha mchezo.

Kwa upande wake Meneja Masoko wa Kampuni ya SBC Sharif Taki alisema kwamba tangu kuanza kudhamini mashindano hayo kwa sasa yamepanua wigo na kuwa na sula ya kitaifa  na tayari yamefanyika Morogoro, Mbeya, Dodoma na wanategemea Arusha kufanyika baada ya kumalizika haya ya Jiji la Mwanza huku pia wakianda ya kukutanisha timu za bingwa kwenye Majiji ya Mwanza, Tanga, Arusha, Mbeya na Dar es salaam.

INASIKITISHA! MBASHA ADAI KUKOMBWA KILA KITU NA FLORA


Imechapishwa na Global TV Jun 25, 2014
Mfanyabiashara na mwimbaji Injili Bongo, Emmanuel Mbasha amesikitishwa na kitendo cha mkewe, Flora Mbasha anayedaiwa kwenda nyumbani na kukomba vitu vya ndani na kuvipeleka kusikojulikana wakati mumewe akisota kwa kesi ya ubakaji.

KIFO CHA MWANAMUZIKI WA FM ACADEMIA KINE DIGITAL CHAWAUMIZA WENGI.

"Umeondoka ukiwa mdogo sana..mpole..mkimya..sauti nzuri..smart..bye Kine Digital..leo nimededicate kipindi kizima cha Tanzania Stars kwako brother...poleni sana Ngwasuma na wapenzi wote wa dansi....one love Dogital..sikiliza wimbo chuki ya nini uisikie sauti yake tamu..aaaghhh" Ameandika Mtangazaji wa Star Tv Bernard James katika ukurasa wake wa facebook.

Mwanamuziki mwenye sauti kali na yenye hisia wa bendi ya FM Academia 'Wazee WaNgwasuma' aitwae Digital amefariki dunia jana ikiwa ni kipindi mfupi tangu alipokuwa amelazwa katika hospital ya Muhimbili jijini Dar, awali tangu wiki iliyopita alikimbizwa hospitali ya Mwananyamala baada ya kuzidiwa na maradhi, na chanzo cha kifo chake hakijaelezwa! poleni FM Academia, ndugu na jamaa katika kipindi hiki kigumu.

Hebu fuatilia video ifuatayo ya wimbo Chuki ya nini ambapo marehemu anaonekana vyema katika dakika ya 6:35
Kwa habari zaidi nitaendelea kuwajuza zaidi, Mungu ailaze mahala pema peponi roho ya marehemu Digital, Ameni!!

CHADEMA JIMBO LA KIGOMA KASKAZINI YATOA TAMKO KUHUSU KUONDOKA KWA WALIOKUWA VIONGOZI WAKE.

CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO; JIMBO LA KIGOMA KASKAZINI
TAMKO KUHUSU KUONDOKA KWA WALIOKUWA VIONGOZI


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Jimbo la Kigoma Kaskazini tunapenda kutoa taarifa kwa umma kutokana na sintofahamu inayotaka kulazimishwa mbele ya jamii kuhusu uimara wa chama chetu mkoani Kigoma.

Tangu jana na leo kumeenea taarifa zinazowahusu watu watatu, Jaffari Kasisiko, Msafiri Wamarwa na Mama Malunga Masoud, ambao vyombo mbalimbali vya habari vimeandika kuwa wamehama chama chetu cha CHADEMA na kukimbilia wanakojua wao (maana CCM inafanya kazi zake katika sura mbalimbali).

Katika hatua ya awali, sisi CHADEMA Jimbo la Kigoma Kaskazini tungependa kusema machache juu suala hilo la watu hao kuhama;
1.      Kwanza watu hao mbali ya kwamba walikuwa ni viongozi wa chama ngazi ya mkoa, kwa uhakika kabisa walikuwa ni kikwazo kama si kizuizi cha muda mrefu sana kwa chama chetu kustawi na kuwa imara zaidi katika mkoa mzima wa Kigoma ili kiweze kukimbizana na wenzetu wa maeneo mengine nchi nzima. Badala yake walikikumbatia na kukiatamia chama. Wakati maeneo mengine wenzetu wakiongeza wabunge majimboni, Kigoma chini ya uongozi wao ikauza majimbo.

2.      Tunaweza kusema kuwa viongozi hawa pamoja na wengine wachache ambao tunajua wako mbioni kuondoka kati ya leo na kesho, walikuwa ni sawa na KOTI LILILOTUBANA. Kwa muda wao wote wa uongozi hawakuwahi kufanya kazi yoyote ya kioganazesheni na kukieneza chama mkoa mzima. Wao walikuwa watu wa mikutano ya hapa na pale Kigoma mjini pekee au pale ambapo kunakuwa na uongozi wa kitaifa au wabunge.

3.      Kwa muda mrefu saa wamekuwa viongozi ‘waliotubana’ kwa sababu walifanya kazi kwa kuangalia zaidi maslahi yao. Sasa kuondoka kwao, ni nafuu kwa chama. Pia ni fursa iliyokuja kwa wakati mwafaka kwa wanachama makamanda waaminifu na watiifu waliofungiwa milango kwa muda mrefu, kusonga mbele kukijenga chama chetu kwa imani kubwa ya kuendelea kubeba matumaini ya Watanzania wanyonge.

4.      Upo ushahidi wa wazi katika hili. Kwa muda mrefu sasa viongozi hao na wengine wenzao waliopangwa kuondoka kwa awamu nyingine, wamekuwa wakilalamikiwa kufanya kazi ya chama kingine cha siasa kwa maslahi na maelekezo ya CCM.

5.      Katika madai yao ya kuhama chama watu hao wamesema wamefikia hatua hiyo eti kutokana na chama chetu kuwa cha kibabe eti kwa sababu tu Zitto Kabwe alivuliwa nafasi Naibu Katibu Mkuu ndani ya chama!

6.      Madai hayo yanashangaza kwa sababu mbali ya chama kuwa na sababu nzito za kumvua Zitto (na wenzake akina Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba) cheo hicho kutokana na tuhuma za utovu wa nidhamu, pia tunaamini hakuna mwanaCHADEMA amejiunga na chama hiki kwa ajili ya cheo. Ndani ya chama chetu tunaamini katika kugawana majukumu si vyeo.

7.      Katika hali ya kushangaza zaidi wanasema eti Zitto amezuiwa kugombea uenyekiti. Sasa tunajiuliza hiyo nia ya kugombea ambayo hatujawahi kuisikia ikitangazwa kwa kufuata katiba, kanuni, maadili, miongozo na itifaki za chama, waliambizana wao wenyewe na mtu wao? Lakini kwa wanachama wa CHADEMA Mkoa wa Kigoma tunaelewa Jafari Kasisiko analipa fadhila za misaada binafsi ikiwemo kupelekwa nje ya nchi.

8.      Ninaomba kutoa wito kwa viongozi wenzangu wa wilaya na majimbo ya Kasulu Mashariki, Muhambwe, Buyungu, Kasulu Magharibi, Manyovu, Kigoma Kaskazini, Kigoma Kusini na Kigoma Mjini, tukutane kwa ajili ya kikao cha Baraza la Mashauriano la Mkoa ili sasa tuchukue hatua zingine za muhimu na haraka za kuhakikisha tunasafisha chama chetu kwa kuwaondoa vibaraka na wasaliti wote waliosalia.

9.      Pia tunaomba katika hali ya dharura Chama Makao Makuu pia kiingilie kwa kutumia kifungu cha Katiba 6.1.3, ili kupata chombo cha kuendelea kuwaunganisha wanachama wakati mkoa ukijiandaa kuchukua hatua hiyo kupitia Baraza la Mashauriano.

10. Sisi wa CHADEMA Kigoma Kaskazini tunawataka wale wengine waliosalia katika mkakati huo wa kuhamisha watu wachache lakini kwa makundi ili eti kujenga taswira ya CHADEMA kubomoka, wakiwemo viongozi kadhaa wa Kanda wasisubiri. Chama chetu kitajengwa na watu wenye imani watakaoweka maslahi na matakwa ya wananchi mbele kwa kuzingatia misingi yetu kama inavyoelezwa katika Katiba ya Chama, kanuni, maadili na miongozo.

Kwa niaba ya Wanachadema imara na makamanda watiifu na waaminifu kwa mabadiliko yanayobeba matumaini na haki za Watanzania wanyonge, naomba kutoa taarifa hii.

Ally Kisala
Mwenyekiti wa CHADEMA Jimbo la Kigoma Kaskazini
Mjumbe wa Baraza la Mashauriano la Mkoa wa Kigoma

Friday, July 18, 2014

UCHAKARIKAJI HAPA NA PALE.

Siku hizi 'Kila kitu Siasa'. 
 Mtembezi.
Kisesa hiyo. 
Bodaboda at Igoma zikisubiri wateja... 
Biashara na soko lisilo rasmi at Igoma.
Huduma za mawasiliano at Igoma.
Matundaz.
Daraja la Mabatini al-Maarufu kwa jina la 'Daraja la Magufuli'
Engo kwa mbaaali.
Mnara wa Nyerere kwenye kipita shoto cha barabara ya Nyerere jijini Mwanza.
Mchapakazi.

AIRTEL YAPUNGUZA GHARAMA ZA MAWASILIANO KWA WAGENI/WATALII

Wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Bw, Sunil Colaso akifuatiwa na  Meneja Masoko wa Airtel bi, Prisca Tembo ,na Mwenyekiti wa shirikisho la  wadau wa Utalii Tanzania Bwana Gaudence Temu , wakionyesha vifurushi vya bidhaa mpya ya Airtel Tourist Pack , wakati wa uzinduzi wa kifurushi hicho kitakacho wawezesha watalii kuwasiliana na familia zao mara wawapo nchi katika utalii, uzinduzi hu umefanyika leo katika makao makuu ya Airtel Daressalaam
Mwenyekiti wa shirikisho la  wadau wa Utalii Tanzania Bwana Gaudence Temu , wakionyesha vifurushi vya bidhaa mpya ya Airtel Tourist Pack , wakati wa uzinduzi wa kifurushi hicho kitakacho wawezesha watalii kuwasiliana na familia zao mara wawapo nchi katika utalii, uzinduzi hu umefanyika leo katika makao makuu ya Airtel Daressalaam.
Mkurgenzi mtendaji wa Airtel Tanzania bw, Sunil Colaso akionyesha waandishi wa habari (hawapo pichani) kifurishi chenye vocha maalum na laini ya Airtel kwaajili ya watalii wanaoingia nchini kitakachojulikana kama Airtel Tourist pack, uzinduzi huo umefanyika leo  ambapo Watalii watakaofaidika ni wale wanaotoka Amerika, India, Italia na Uingereza kufaidika na 'Airtel Tourist pack'
Airtel yaja na 'Tourist pack' yashusha gharama za simu na Intaneti kwa Watalii

*        Watalii toka Amerika, India, Italia na Uingereeza kufaidika na 'Airtel Tourist pack'
*        Airtel yapunguza gharama za kupiga simu na intaneti kwa watalii  toka Amerika, India, Italia na Uingereeza
Dar es Saalam, Juni 17, 2014, Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel leo imekuja na ubunifu mpya wa bidhaa itakayojulikana kama AIRTEL TOURIST PACK maalum kwa wageni/watalii wanaotembelea nchini toka mataifa mbalimbali ikiwa ni muendelezo wa Airtel kuendelea kutoa huduma bora ya mawasiliano nafuu kwa kuwaweza kuwasiliana na ndugu na familia zao wawapo kwenye utalii wao.

Akiongea wakati wa uzinduzi wa huduma hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Bw, Sunil Colaso alisema" Huduma hii mpya ya "Vifurushi vya watalii" itapunguza usumbufu kwa mtalii/mgeni kukosa mawaliano bora ya simu au Intaneti awapo katika sehemu mbalimbali ya vivutio vya utalii nchini.

Ni imani yangu kuwa wageni watafurahia huduma hii kutokana na ubora wa mawasilano ya Airtel hasa katika maeneo ya pembezoni mwa miji ambako ndiko vivutio vingi vya utalii vinakopatika.

"Kifurushi hiki cha watalii kitakuwa na muda wa maongezi  wa dakika 30 za kupiga simu za nje, dakika 10 za kupiga simu za ndani ya nchi, SMS 10 kwenda mtandao wowote ndani na nje ya nchi pamoja na kifurushi cha intaneti cha 1GB vitakavyodumu kwa muda wa siku 30" alieleza Bw, Colaso

Kifurushi cha watalii Airtel Tourist Pack pia kinakuja na Laini ya simu na vocha ambapo, hii ni kwa yule mteja ambae hana laini ya Airtel au anataka kujiunga na kufaindika na huduma

Mtumiaji wa "Kifurushi cha watalii" Airtel Tourist pack atatakiwa kusajili namba yake pale tu anapofanya manunuzi kwa kutoa kitambulisho au pasi ya kusafiria.  Usaliji huo utakuwa wa muda kwa siku 30 na baada ya hapo mtalii atatakiwa kutoa kopi ya kitambulisho au pasi ya kusafiria kwaajili ya usajili wa kudumu.

Huduma hii ya vifurushi kwa wageni wakutoka nje ya nchi kwa simu ni ya kwanza kutoka Airtel na inampatia mteja uhuru wa kuwasilina  na ndugu jamaa na marafiki nyumbani kwa gharama nafuu zaidi kuliko ilivyokuwa awali, wateja watafurahia huduma za internet kwa kujiunga na mitandao ya kijamii, kutuma picha na video kwa gharama nafuu wakati wote . Aliongeza Colaso

Kwa upande wake mgeni rasmi, Mwenyekiti wa wadau wa Utalii nchini Bw, Gaudence Temu alisema "kwa niaba ya wadau wote wa utalii, ninaipongeza sana Airtel kwa kuanzisha huduma hii ya vifurushi vya mawasiliano kwa watalii wanaoingi nchini. Huduma hii inaendana na mahitaji ya wageni wetu na inakwenda sambamba na dhamira yetu sisi wadau ya kuendelea kutoa huduma bora katika soko.

"kwa kupitia mtandao wa Airtel ulioenea zaidi maeneo ya vijijini wageni wetu sasa watakuwa na uhakika wa mawasiliano bora na kwa gharama nafuu wakati wote" alieleza Bw, Temu

Mwenyekiti huyo pia alitoa ushauri kwa wadau wote wa biashara ya utalii kuchangamkia fulsa hiyo kwa kuwajulisha wageni wanaoingia nchini ili waweze kufaidika na punguzo hilo ambalo kwa msimu huu wa utalii hutumia gharama kubwa katika mawasiliano.

"Migahawa na Hoteli, wadau wa usafirishaji, watembezaji watalii na wadau wote hii ni fulsa kwetu kuwapa habari njema wateja wetu wanapoingia nchini kwamba kuna Tourist pak yenye faida zote hizi" alimaliza kwa kusema Bw, Temu

Vifurushi vya watalii zitapatikana katika maeneo yote ya biashara katika maeneo ya kuingia nchini kama zile viwanja vya ndege vya Dar es saalam(JKIA), Zanzibar, Arusha na KIA. Pia zinapatikana katika hoteli na migahawa ya kitalii.

Nchi zitakazofaidika na huduma hii kwa sasa ni pamoja na Amerika, India, Italia na Uingereeza.

KATIKA PICHA AJALI YA NDEGE YA MALAYSIA ILIYOUWA WATU 295.

Ndege ya shirika la Malaysian ikiwa na abiria 295 imeanguka Mashariki mwa Ukraine ikiwa safarini kutoka Amsterdam hadi Kuala Lumpur kukiwa na madai kwamba ilidunguliwa.
Rais wa Ukraine alielezea tukio hilo kuwa ni tendo la kigaidi huku waasi wakikanusha kuidungua. Inaaminiwa waasi hao wanaotaka kujitenga walizidungua ndege mbili za jeshi la Ukraine katika eneo hilo hivi karibuni.
Mabaki ya ndege hiyo ya shirika la Malaysian iliyoanguka na kuuwa abiria 295 .
Miili ya watu imetapakaa kila upande katika kile kinachoaminika kuwa masalia ya ndege hiyo ya muundo wa jet karibu na kijiji cha Grabovo, kinachodhibitiwa na waasi wanaotaka kujitenga,.
Ndege hiyo nambari MH17 ilikua inakaribia kuingia anga ya Urusi mawasiliano yalipokatizwa.
Passport zimebaki kama kumbukumbu na vielelezo vya abiria waliofariki dunia kwenye ajali hiyo.
Miili ya wahanga wa ndege hiyo, mizigo pamoja na mabaki ya ndege hiyo imetawanyika eneo la ajali. 
Anga ya Ukraine haikufungwa rasmi lakini mashirika ya ndege ya Ujerumani, Lufthansa, Air France ya Ufaransa na Uturuki,yanaliepuka eneo la Ukraine Mashariki.

WAJUMBE WA BUNGE LA KATIBA WATAKIWA KUWA NA MTIZAMO MPYA UTAKAOWEZESHA

Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Bw. Deus Kibamba akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika leo Julai 17, 2014 kuelezea msimamo wa JUKWAA LA KATIBA juu ya mwenendo uliopita wa bunge hilo. Picha na Cathert Kajuna wa Kajunason Blog.
Kiongozi wa Shule Kuu ya Sheria nchini Kenya, Profesa Patrick Lumumba alisisitiza suala la wanasiasa kurudi bungeni na kuhakikisha katiba mpya inapatikana.
Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia mkutano huo.
Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia mkutano huo.
Wajumbe wa JUKWAA LA KATIBA wakisisitiza jambo.
Wajumbe wa JUKWAA LA KATIBA wakisisitiza jambo.
Na Hellen Kwavava, Dar es Salaam.
Ushauri Umetolewa kwa Wajumbe wa Bunge Maalum la katiba kuwa na Mtazamo mpya utakaoiletea nchi maslahi pindi watakaporudi bungeni katika mchakato wakutafuta katiba mpya unaotarajiwa kuanza mapema mwezi ujao.

Hata hivyo kundi la Umoja wa katiba ya wananchi (UKAWA) limezidi kushauri wakirudi bungeni na kuendelea na majadiliano kwa msingi wa rasimu ya katiba.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam leo Julai 17, 2014 na mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Bw. Deus Kibamba ambapo ameeleza kwamba wabunge wanatakiwa kuachana na mtazamo wa kisiasa pamoja na lugha zisizo na staa kwenye bunge hilo kwani wanatakiwa kuzingatia uzalendo kwanza.

Aidha Bw. Kibamba amesema kwamba licha ya muda kuwa mfupi kuelekea katika uchaguzi wa mwaka 2015 wao wanapendekeza juhudi zaidi zifanyike ili kukamilisha upatikanaji wa katiba hiyo.

Naye Kiongozi wa shule kuu ya Sheria nchini Kenya Profesa Patrick Lumumba amewasihi wanasiasa wa nchini kuhakikisha katiba inapatikana kutokana na matakwa ya wananchi kwani nchini jirani zimekuwa zikiiga mambo mengi kutoka huku.

Bunge Maalum la katiba linatajiwa kuanza tena Agosti 5, 2014 mwaka huu.

Thursday, July 17, 2014

SASA WANANCHI KUWASILISHA MALALAMIKO YA WATENDAJI WABOVU SERIKALINI KUPITIA SIMU ZA VIGANJANI.

Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Bi. Marry Massay akiwasilisha moja kati ya mada za uboreshaji katika upokeaji taarifa za malalamiko ya utendaji mbovu wa watumishi wa Serikali, mtu mmoja mmoja, makampuni na mashirika mengine binafsi, ambapo kwa sasa Tume hiyo imetambulisha namba maalum ya mawasiliano ya simu ya mkononi iliyo rasmi kwaajili ya kupokea malalamiko kwa njia ya ujumbe mfupi yaani sms na kufanyia kazi. 
Kwa mujibu wa Bw. Wilfred Warioba ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha IT amesema kuwa Semina hiyo imelenga kuzidisha uelewa wa asasi zisizo za kiserikali kuhusiana na jinsi ya kuwasilisha malalamiko mbele ya Tume ya haki za binadamu na utawala bora, ambapo mlalamikaji anapata fursa ya kuwasilisha malalamiko yake kwa njia rahisi zaidi kupitiasimu yake ya kiganjani.
Wilfred Warioba, alisema ili kurahisisha mawasiliano ya tume hiyo na wananchi, Tume imeamua kuanzisha teknolojia hiyo ya kutuma malalamiko moja kwa moja kupitia mitandao ya simu zao kwa njia ya ujumbe mfupi yaani ‘sms’. 

Aliongeza kuwa tume ya haki za binadamu na utawala bora ni chombo huru ambacho kiko kwa ajili ya kutetea wananchi wote na hakitozi gharama yoyote ya kuwasilisha malalamiko. 

Mtaalamu huyo aliongeza kuwa tume inapokea malalamiko ya aina yoyote ile bila kujali yameletwa na nani ili mradi yawe na ukweli ndani yake, kinachotakiwa ni mhusika kuandika malalamiko yake kwenye sehemu ya kuandika ujumbe mfupi kwenye simu yake ya mkononi na kisha kuutuma kwenye namba 0754 460 256. 

Ujumbe huo ukishapokelewa mhusika (mlalamikaji) atapigiwa simu na kuulizwa baadhi ya mambo ili kujua kiini cha malalamiko yake kwa lengo la kujiridhisha ikiwa ni pamoja na kufahamu anaitwa nani, yuko wapi na mambo mengine yatakayoturahisishia kushughulikia malalamiko yake kwa wepesi zaidi, aliongeza.

Aidha Warioba alisema mwananchi yeyote atakayeleta malalamiko yake kwa ‘sms’ anatakiwa kutumia majina yake halisi na kutaja mahali alipo na si kusema uongo lengo likiwa kurahisisha kazi ya kushughulikia malalamiko yake. 

Alifafanua kuwa tume hii haina upendeleo wowote wa kijinsia katika kushughulikia malalamiko ya wananchi yanayopokelewa huku akibainisha kuwa wananchi walio wengi  bado hawajajua wajibu wao kwani wanayo matatizo mengi ila wanayanyamazia tu ndio maana tumewatembelea ili waseme waziwazi. 

Afisa Mfawidhi Mkoa wa Mwanza Albert Kakenke akitoa ufafanuzi kwa washiriki.
Ndani ya semina na washiriki toka asasi mbalimbali za kiraia.

Kwa umakiiiini hii ni sehemu ya washiriki wa semina hiyo.
Washiriki.
Semina ikiendelea.
Tume ya uwasilishaji wa malalamiko kwa njia ya 'SMS' imeanzishwa mnamo mwezi Julai 2001 hapa nchini ikiwa imelenga kulinda na kutetea maslahi ya wananchi ambapo imejiwekea utaratibu wa kupokea na kushughulikia malalamiko mbalimbali ya wananchi kuanzia ngazi ya serikali kuu mpaka ngazi ya vijiji.  ‘Mpaka sasa tume hiyo ina ofisi katika kanda  4 tu ambazo ni Lindi, Mwanza, DSM na Zanziba, lengo letu ni kuelimisha umma ili wafahamu wajibu wao ni nini, haki zao ni zipi, wanawezaje kuzipata na kwa utaratibu gani’, aliongeza Shayo.

Picha ya pamoja wadau wa Tume na wadau wa asasi mbalimbali za kiraia jijini Mwanza.

Wednesday, July 16, 2014

NAIBU WAZIRI WA WIZARA YA HABARI,VIJANA,NA MICHEZO AZINDUA RASMI KITABU CHA 'HISTORIA YA KLABU YA SIMBA' KILICHO ANDIKWA NA MWINA KADUGUDA.





 Mwina Kaduguda Mtunzi wa kitabu cha "HISTORIA YA SIMBA" akielezea kwa kina Magumu gani amepitia wakati anaanza kuandaa kitabu hicho,Wa kwanza Kushoto ni Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia na Katikati ni Mkurugenzi wa Mkuki na Nyota Bwana Mkuki Bgoya ambao ndio wachapishaji wa kitabu hicho.Akielezea kwa ufupi Mwina Kaduguda amesema kwamba Dhumuni kubwa la Kutunga kitabu hicho ni kutaka kutunza historia ya soka ya Timu hiyo isipoteee ili iweze kusomwa kizazi na kizazi.





 Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia Akijiandaa kukata utepe ili kuweza kuzindua rasmi kitabu hicho cha historia ya Simba,Wanaoshuhudia kulia ni mtunzi wa kitabu hicho Mwina Kaduguda akifuatiwa na Bwana Mkuki Bgoya mkurugenzi wa Mkuki na Nyota Ambao ndio wachapishaji wa kitabu hicho



Mkurugenzi wa Mkuki na Nyota Bwana Mkuki Bgoya  Akielezea namna walivyochapa kitabu hicho na ubora wake .



 Mjumbe wa kamati ya Utendaji Klabu ya Simba Bwana Collin Frisch akiongea kwa niaba ya Rais wa Simba,ambapo amempongeza sana Mwina Kaduguda na kusema ameiweka Klabu ya Simba kwenye Kumbukumbu muhimu sana kwenye soka la Tanzania hivyo inatakiwa aungwe mkono kwa nguvu zote.


Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia akitoa neno kumpongeza Mwina Kaduguda  kwa kufikiria mbali sana kwa kuweka soka la Tanzania kwenye maandishi namna klabu ya simba ilivyoanza, Akaongeza kuwa Klabu za soka Tanzania zinatakiwa kuwa na watu kama Mwina Kaduguda ili kuleta maendeleo ya soka.Naibu waziri pia akasisitiza ni wakati wa kila mwanachama kujituma kwa bidii na kuacha kukaaa kwenye korido za Klabu na kupiga Zoga.


Mwina kaduguda Mtunzi wa Kitabu cha "HISTORIA YA SIMBA" Akimkabidhi  Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia Zawadi ya Kitabu ambayo ameomba apelekewe Rais Jakaya Mrisho Kikwete.


Mwina kaduguda Mtunzi wa Kitabu cha "HISTORIA YA SIMBA" Akimkabidhi  Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia Zawadi yake ya Kitabu.


Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Klabu ya Simba Collin Frisch akiwa na Mtunzi wa kitabu cha Historia ya Simba Mwina Kaduguda kwenye uzinduzi Rasmi wa kitabu hicho kwenye ukumbi wa Klabu ya Simba.


Wageni waalikwa waliokuja Kushuhudia Uzinduzi wa Kitabu cha "HISTORIA YA SIMBA" Kutoka kulia ni Fredrick Mwakalebela,Said Tulliy(Mjumbe wa kamati ya Utendaji),Hassan Dalali(mwenyekiti Mstaafu) na Mtunzi wa kitabu Hicho Mwina Kaduguda.


Wapenzi,wanachama wa Simba Pamoja na Vyombo vya habari waliohudhuria Uzinduzi wa Kitabu cha "HISTORIA YA SIMBA" wakifuatilia kwa makini Uzinduzi huo.


Hizo ni kopi za Kitabu cha "HISTORIA YA SIMBA" kilichozinduliwa leo na Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia.