ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, July 19, 2014

CHADEMA JIMBO LA KIGOMA KASKAZINI YATOA TAMKO KUHUSU KUONDOKA KWA WALIOKUWA VIONGOZI WAKE.

CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO; JIMBO LA KIGOMA KASKAZINI
TAMKO KUHUSU KUONDOKA KWA WALIOKUWA VIONGOZI


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Jimbo la Kigoma Kaskazini tunapenda kutoa taarifa kwa umma kutokana na sintofahamu inayotaka kulazimishwa mbele ya jamii kuhusu uimara wa chama chetu mkoani Kigoma.

Tangu jana na leo kumeenea taarifa zinazowahusu watu watatu, Jaffari Kasisiko, Msafiri Wamarwa na Mama Malunga Masoud, ambao vyombo mbalimbali vya habari vimeandika kuwa wamehama chama chetu cha CHADEMA na kukimbilia wanakojua wao (maana CCM inafanya kazi zake katika sura mbalimbali).

Katika hatua ya awali, sisi CHADEMA Jimbo la Kigoma Kaskazini tungependa kusema machache juu suala hilo la watu hao kuhama;
1.      Kwanza watu hao mbali ya kwamba walikuwa ni viongozi wa chama ngazi ya mkoa, kwa uhakika kabisa walikuwa ni kikwazo kama si kizuizi cha muda mrefu sana kwa chama chetu kustawi na kuwa imara zaidi katika mkoa mzima wa Kigoma ili kiweze kukimbizana na wenzetu wa maeneo mengine nchi nzima. Badala yake walikikumbatia na kukiatamia chama. Wakati maeneo mengine wenzetu wakiongeza wabunge majimboni, Kigoma chini ya uongozi wao ikauza majimbo.

2.      Tunaweza kusema kuwa viongozi hawa pamoja na wengine wachache ambao tunajua wako mbioni kuondoka kati ya leo na kesho, walikuwa ni sawa na KOTI LILILOTUBANA. Kwa muda wao wote wa uongozi hawakuwahi kufanya kazi yoyote ya kioganazesheni na kukieneza chama mkoa mzima. Wao walikuwa watu wa mikutano ya hapa na pale Kigoma mjini pekee au pale ambapo kunakuwa na uongozi wa kitaifa au wabunge.

3.      Kwa muda mrefu saa wamekuwa viongozi ‘waliotubana’ kwa sababu walifanya kazi kwa kuangalia zaidi maslahi yao. Sasa kuondoka kwao, ni nafuu kwa chama. Pia ni fursa iliyokuja kwa wakati mwafaka kwa wanachama makamanda waaminifu na watiifu waliofungiwa milango kwa muda mrefu, kusonga mbele kukijenga chama chetu kwa imani kubwa ya kuendelea kubeba matumaini ya Watanzania wanyonge.

4.      Upo ushahidi wa wazi katika hili. Kwa muda mrefu sasa viongozi hao na wengine wenzao waliopangwa kuondoka kwa awamu nyingine, wamekuwa wakilalamikiwa kufanya kazi ya chama kingine cha siasa kwa maslahi na maelekezo ya CCM.

5.      Katika madai yao ya kuhama chama watu hao wamesema wamefikia hatua hiyo eti kutokana na chama chetu kuwa cha kibabe eti kwa sababu tu Zitto Kabwe alivuliwa nafasi Naibu Katibu Mkuu ndani ya chama!

6.      Madai hayo yanashangaza kwa sababu mbali ya chama kuwa na sababu nzito za kumvua Zitto (na wenzake akina Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba) cheo hicho kutokana na tuhuma za utovu wa nidhamu, pia tunaamini hakuna mwanaCHADEMA amejiunga na chama hiki kwa ajili ya cheo. Ndani ya chama chetu tunaamini katika kugawana majukumu si vyeo.

7.      Katika hali ya kushangaza zaidi wanasema eti Zitto amezuiwa kugombea uenyekiti. Sasa tunajiuliza hiyo nia ya kugombea ambayo hatujawahi kuisikia ikitangazwa kwa kufuata katiba, kanuni, maadili, miongozo na itifaki za chama, waliambizana wao wenyewe na mtu wao? Lakini kwa wanachama wa CHADEMA Mkoa wa Kigoma tunaelewa Jafari Kasisiko analipa fadhila za misaada binafsi ikiwemo kupelekwa nje ya nchi.

8.      Ninaomba kutoa wito kwa viongozi wenzangu wa wilaya na majimbo ya Kasulu Mashariki, Muhambwe, Buyungu, Kasulu Magharibi, Manyovu, Kigoma Kaskazini, Kigoma Kusini na Kigoma Mjini, tukutane kwa ajili ya kikao cha Baraza la Mashauriano la Mkoa ili sasa tuchukue hatua zingine za muhimu na haraka za kuhakikisha tunasafisha chama chetu kwa kuwaondoa vibaraka na wasaliti wote waliosalia.

9.      Pia tunaomba katika hali ya dharura Chama Makao Makuu pia kiingilie kwa kutumia kifungu cha Katiba 6.1.3, ili kupata chombo cha kuendelea kuwaunganisha wanachama wakati mkoa ukijiandaa kuchukua hatua hiyo kupitia Baraza la Mashauriano.

10. Sisi wa CHADEMA Kigoma Kaskazini tunawataka wale wengine waliosalia katika mkakati huo wa kuhamisha watu wachache lakini kwa makundi ili eti kujenga taswira ya CHADEMA kubomoka, wakiwemo viongozi kadhaa wa Kanda wasisubiri. Chama chetu kitajengwa na watu wenye imani watakaoweka maslahi na matakwa ya wananchi mbele kwa kuzingatia misingi yetu kama inavyoelezwa katika Katiba ya Chama, kanuni, maadili na miongozo.

Kwa niaba ya Wanachadema imara na makamanda watiifu na waaminifu kwa mabadiliko yanayobeba matumaini na haki za Watanzania wanyonge, naomba kutoa taarifa hii.

Ally Kisala
Mwenyekiti wa CHADEMA Jimbo la Kigoma Kaskazini
Mjumbe wa Baraza la Mashauriano la Mkoa wa Kigoma

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.